BREAKING

Monday 23 July 2018

SIMBA WAANZA KUJIFUA UTURUKI CHINI YA KOCHA MPYA MBELGIJI PATRICK AUSSEMS




Kikosi  cha Simba SC kimewasili salama mjini Istanbul, Uturuki baada ya kuondoka Aflajiri ya Jumapili kuweka kambi ya muda wa wiki mbili kujiandaa na Ligi Kuu ya Tanzania bara inayotarajiwa kuanza Agosti 22, mwaka huu.

Na mara baada ya kuwasili, Simba SC walipumzika kidogo kabla ya kwenda kufanya mazoezi yao ya kwanza jioni ya leo Istanbul ambayo pia yalikuwa mazoezi ya kwanza chini ya kocha mpya, Mbelgiji Patrick J Aussems. 

Simba SC imeondoka na wachezaji wote iliyowasajili kwa ajili ya msimu ujao chini ya kocha wake mpya Aussems atakayekuwa chini ya Msaidizi Mrundi, Masoud Juma aliyekuwa Msaidizi pia wa makocha wawili waliopita, Mcameroon Joseph Omog na Mfaransa, Pierre Lechantre.

Ikiwa nchini Uturuki, Simba SC itapata mazoezi katika mazungira na viwanja bora, pamoja na mechi za kirafiki za kujipima nguvu kabla ya kurejea nchini kwa ajili ya tamasha la Simba Day Agosti 8 Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.

Ikumbukwe Simba SC, mabingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania watauanza msimu kwa mchezo wa wa Ngao ya Jamii dhidi ya washindi wa Kombe la Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), maarufu Azam Sports Federation Cup (ASFC), Mtibwa Sugar Agosti 18, mwaka huu Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza.  
             
Katika Ligi Kuu, Simba itaanza na Tanzania Prisons Agosti 22, mechi itakayochezwa Saa 1:00 usiku Uwanja wa Taifa mjini Dar es Salaam.

Na watakutana na mahasimu wao wa jadi, Yanga watakutana Septemba 30, mwaka huu katika mechi ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara kuanzia Saa 10:00 jioni Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

 
Copyright © 2016 Shamakala
Designed by Switch International | SHAMAKALA 360
    Twitter Facebook Google Plus Vimeo Videosmall Flickr YouTube