BREAKING

Thursday 16 March 2017

AHMED AHMED AMALIZA UTAWALA WA MIAKA 29 WA ISSA HAYATOU, CAF



Ahmed Ahmed kuchaguliwa kwa kishindo na kumuangusha Issa Hayatou, 

 Barani Afrika, Caf, hatimaye limepata rais mpya baada ya Ahmed Ahmed kuchaguliwa kwa kishindo na kumuangusha Issa Hayatou, moja ya viongozi wakongwe zaidi waliowahi kuhudumu kwa muda mrefu kwenye taasisi ya soka.

Ahmed amemshinda Hayatou kwa kura 34 kwa 20 katika uchaguzi ambao sasa unamaliza miaka 29 ya utawala wa Hayatou aliyekuwa akiongoza shirikisho hilo la mpira barani Afrika toka mwaka 1988.

Ahmed, mwenye umri wa miaka 57 na baba wa watoto wawili, amekuwa kwa muda akifundisha soka na kucheza mpira kwa nyakati tofauti kabla ya kuchukua urais wa chama cha soka cha Madagascar mwaka 2003.

Uchaguzi wa mwaka huu umekuwa wa kihistoria kwa kuwa ni mara ya kwanza kwa Issa hayatou kupata upinzani mkali ukilinganisha na chaguzi nyingine zilizotangulia ambapo mara zote amekuwa akipitishwa kwa kishindo na wakati mwingine kukosa mpinzani.

Toka kutangaza kuwa atawania kiti cha urais kwenye uchaguzi wa mwaka huu, Ahmed alipata mara moja uungwaji mkono kutoka kwa baadhi ya viongozi wa mashirikisho ya soka barani Afrika, ambao walipenda sera za mgombea huyu aliyekuwa akijinasibu kufanya mabadiliko makubwa kwenye shirikisho hilo la kulibadili soka la Afrika.

Mwaka huu mara kadhaa imeshuhudiwa Issa Hayatou akiingia kwenye mvutano wa maneno na marais wa vyama vya soka toka nchi za kusini mwa Afrika COSAFA, ambao wao toka awali waliweka wazi msimamo wao kuhusu kumuunga mkono Ahmed Ahmed.

Uchaguzi wa mwaka huu pia umekuwa na mvuto wa aina yake, kwakuwa hata baadhi ya vyama vya soka ambavyo kwa miaka nenda rudi vimekuwa vikimuunga mkono Issa Hayatou kwenye chaguzi zilizopita, walibadili kibao na kutangaza hadharani kutomuunga mkono.

Ahmed Ahmed, mgombea ambaye awali alikuwa hapewi sana nafasi ya kumshinda Hayatou kwenye uchaguzi wa mwaka huu, alipata umaarufu na uungwaji mkono toka kwa baadhi ya viongozi wa soka baada ya kuonekana kuwa na ahadi muhimu ya kulibadili soka la Afrika.

No comments:

Post a Comment

 
Copyright © 2016 Shamakala
Designed by Switch International | SHAMAKALA 360
    Twitter Facebook Google Plus Vimeo Videosmall Flickr YouTube