BREAKING

Tuesday 30 August 2022

MAKAMU WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA DKT. PHILIP MPANGO AFANYA MAZUNGUMZO NA BALOZI WA SINGAPORE NCHINI TANZANIA


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akifanya mazungumzo na Balozi wa Singapore nchini Tanzania Mhe. Douglas Foo, Mazungumzo yaliofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma leo Tarehe 30 Agosti 2022






Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Singapore nchini Tanzania Mhe.Douglas Foo mara baada ya Mazungumzo yaliofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma leo Tarehe 30 Agosti 2022

Na Mwandishi wetu Ofisi ya Makamu wa Rais..

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Mpango leo tarehe 30 Agosti 2022 amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Singapore nchini Tanzania Mhe. Douglas Foo, Mazungumzo yaliofanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma.

 Katika Mazungumzo hayo, Makamu wa Rais amesema Tanzania ipo tayari kushirikiana na Singapore katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya Bandari, Afya, Viwanda, Elimu, Kilimo, Biashara, Uchumi wa Buluu pamoja na Tehama kupitia uwekezaji katika vifaa vya kielekroniki.

 Amesema serikali ya awamu ya sita imeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara hapa nchini ikiwa ni pamoja kushirikiana na mataifa katika masuala mbalimbali na kuhakikisha sera zilizopo ni thabiti na zisizobadilika badilika.

 Makamu wa Rais amesema serikali imeweka mkazo katika kuboresha rasilimali watu ikiwemo kuhakikisha elimu ya msingi na sekondari inatolewa bila malipo, kujenga miundombinu ya elimu pamoja na msisitizo wa elimu ya sayansi husasani kwa wanafunzi wa kike. Pia amesema uwekezaji unafanyika katika sekta ya afya, upatikanaji wa maji safi na salama, ujenzi wa miundombinu ya barabara kuunganisha mikoa na vijiji, kuhakikisha upatikanaji wa nishati pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa.

 Halikadhalika, Makamu wa Rais amewakaribisha wawekezaji kutoka nchini Singapore kuwekeza katika sekta mbalimbali nchini ikiwemo katika miundombinu ya utalii, kuwekeza katika viwanda na teknolojia rafiki za kuongeza thamani ya mazao ya kilimo pamoja na madini. Aidha amesema kutokana na mafanikio yaliopatikana nchini Singapore katika sekta ya bandari, ipo haja ya kuongeza ushirikiano utakaowezesha mafunzo ya watendaji wa Bandari pamoja  upatikanaji wa mitambo ya kisasa.

 Kwa Upande wake Balozi wa Singapore nchini Tanzania Mheshimiwa Douglas Foo amesema Singapore inatarajia kuongeza ushirikiano na Tanzania katika maeneo mbalimbali hususani biashara na uwekezaji. Ameongeza kwamba kutokana na nchi hiyo  kuwa eneo dogo kwaajili ya shughuli za kilimo hivyo ipo tija kubwa katika ushirikiano na Tanzania kwenye sekta hiyo itakayowezesha kuongezwa thamani ya mazao na kufikia soko la nchi hiyo na nchi zinginezo za bara la Asia.

 Aidha ameikaribisha Tanzania kushirikiana na Singapore katika sekta ya utalii, Uvuvi na uchumi wa Buluu kwa ujumla. Amesema nchi hiyo sekta ya uzalishaji wa viwandani inachangia asilimia 20 katika pato la taifa hivyo ipo tayari kushirikiana na Tanzania kwa kuanzisha viwanda vya uzalishaji pamoja na kutoa elimu ya ufundi hapa nchini itakayoongeza tija katika viwanda hivyo

Pia Amesema Singapore imeendelea na uwekezaji katika teknolojia unaorahisisha ufanyaji kazi pamoja na ufuatiliaji wa masuala mbalimbali ikiwemo masuala ya kiafya na kielimu. Ameongeza kwamba nchi hiyo imeweka mkazo katika utunzaji wa mazingira ikiwemo kuwaka faini kubwa kwa wachafuzi wa mazingira huku ikitarajia kuondoa kabisa uzalishaji wa hewa ukaa ifikapo mwaka 2050. 

MKOMI: LINDENI MALIASILI ZA TAIFA


Naibu Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii, Juma Mkomi akizungmza na Wahifadhi wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo Wenyeviti wa Sekretarieti na Maafisa wa Kanda kumi za kiikolojia katika nyanja za intelijensia, uchunguzi na mashtaka ambapo amewataka mafunzo watakayoyapata wayatafsiri kwa vitendo. 

Baadhi ya Wenyeviti wa Kanda za Kiikolojia wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii, Juma Mkomi wakati akifungua mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo Wahifadhi katika nyanja za intelijensia, uchunguzi na mashtaka.

Naibu Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii, Juma Mkomi (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Sekretarieti ya Mafunzo akizungmza  ya kuwajengea uwezo Wenyeviti wa Sekretarieti na Maafisa wa Kanda kumi za kiikolojia mara baada ya kufungua mafunzo hayo.

NAIBU Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii, Juma Mkomi amewataka Wahifadhi  kwenda kusimamia jukumu ya msingi la Wizara ya Maliasili na Utalii  ambalo ni kulinda na kuhifadhi maliasili za Taifa ikiwemo Misitu na Wanyamapori

 Mkomi  ameyasema hayo leo Jumanne Agosti 30, 2022  Jijini Arusha wakati akifungua mafunzo ya kuwajengea uwezo Wenyeviti wa Sekretarieti na Maafisa wa Kanda kumi za kiikolojia katika nyanja za intelijensia, uchunguzi na mashtaka

Mafunzo hayo yanayofanyika kwa muda wa siku mbili kuanzia leo yamehudhuriwa na  Washiriki kutoka  Jeshi la Polisi nchini ,  Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Wahifadhi  kutoka TANAPA, NCAA, TAWA na TFS, 

Akizungumza wakati akifungua mafunzo hayo, Mkomi amesema Wahifadhi  wana wajibu wa kushirikiana na vyombo vingine vya usalama  katika kuwabaini majangili wa wanyamapori na Misitu

Amewataka Washiriki hao kuzingatia mafunzo hayo   na kwenda kuyafanyia kazi kwa kuhakikisha Wahalifu wa wanyamapori na misitu wanakamatwa kabla ya kuharibu Maliasili zetu.  

“ Mafunzo hayo mtakayopewa yakawe chachu katika kuchagiza utalii hivi sasa  filamu ya Royal Tour  imeitangaza vizuri nchi yetu na  Watalii wameanza kumiminika nchini kutokana na kazi kubwa mnayofanya ninyi Wahifadhi msingekuwa mmefanya kazi kubwa kulinda wanyamapori watalii wasingekuja kwa sababu kusingekuwa na wanyamapori ,” amesema.

Kutokana na jukumu walilonalo la kulinda Maliasili, Naibu Katibu Mkuu, Mkomi amewataka wahifadhi hao kuzingatia mafunzo hayo hususani suala la uchunguzi kwa kujifunza mbinu za kuzuia uharibifu wowote unaoweza kutokea kwenye maeneo ya hifadhi 

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Wanyamapori, Dkt. Maurus Msuha  amesema suala la Uhifadhi linakabiliwa na changamoto ya usimamizi wa Maliasili hivyo  mafunzo hayo yakalete majawabu katika kulinda maliasili

Pia Dkt. Msuha amesema  mafunzo hayo  yanakwenda kuboresha utendaji kazi kwa kuhakikisha uhalifu wa wanyamapori na Misitu litachochea ufanisi zaidi katika utendaji w kazi wa kulinda maliasili zetu.

Naye Mratibu wa Mafunzo hayo ambaye pia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Wanyamapori, Robert Mande amesema mafunzo hayo ni muendelezo wa kukumbushana namna ya kushughulika na waharifu wa wanyamapori wa misitu mara wanapokamtwa.

“Lazima tuhakikishe kuwa tunalinda rasilimali za wanyamapori ili watalii wanavyokuja waweze kuziona na waweze kuwa na usalama”Mande amefafanua.

RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA SAMIA SULUHU HASSAN AFUNGUA KIKAO KAZI CHA MAAFISA WAKUU WA POLISI


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati akifungua Kikao Kazi Cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Makao Makuu ya Polisi na Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Vikosi kilichofanyika katika Chuo cha Polisi (CCP) Mkoani Kilimanjaro tarehe 30 Agosti, 2022.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akiwa na viongozi wengine katika picha ya pamoja na Maafisa Wakuu Waandamizi wa Makao Makuu ya Polisi na Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Vikosi mara baada ya kufungua Kikao Kazi cha Makamanda hao kilichofanyika kwenye Chuo cha Polisi (CCP) Mkoani Kilimanjaro tarehe 30 Agosti, 2022.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akizungumza wakati akifungua Kikao Kazi Cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Makao Makuu ya Polisi na Makamanda wa Polisi wa Mikoa na Vikosi kilichofanyika katika Chuo cha Polisi (CCP) Mkoani Kilimanjaro tarehe 30 Agosti, 2022.







Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Mhe. Samia Suluhu Hassan akiagana na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Nurdin Babu mara baada ya kufungua Kikao Kazi cha Makamanda hao kilichofanyika kwenye Chuo cha Polisi (CCP) Mkoani Kilimanjaro tarehe 30 Agosti, 2022.


 

 
Copyright © 2016 Shamakala
Designed by Switch International | SHAMAKALA 360
    Twitter Facebook Google Plus Vimeo Videosmall Flickr YouTube